APRM Tanzania yashirikiana na Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana na Wadau kufanikisha Vijana Uchumi Challenge 2026
Taasisi ya African Peer Review Mechanism (APRM) Tanzania imeshirikiana na Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, National Social Security Fund (NSSF), UTT Asset Management and Investor Services (UTT AMIS), Tanzania Communications Regulatory Authority (TCRA), WCF, Save the Children Tanzania, African Leadership Initiatives for Impact, CRDB Bank Foundation, NMB Bank na iMbeju kufanikisha Vijana Uchumi Challenge 2026 kupitia udhamini na ushiriki katika mchakato mzima wa mashindano kuanzia hatua za awali hadi fainali. Mashindano hayo yalilenga kuibua na kukuza bunifu za vijana zenye uwezo wa kutoa suluhisho kwa changamoto za maendeleo, kuchochea ubunifu na kuimarisha ukuaji wa uchumi nchini.
Vijana Uchumi Challenge imeendelea kujidhihirisha kama shindano linalowapa vijana nafasi ya kuwasilisha mawazo bunifu yanayoweza kutoa suluhisho kwa changamoto za maendeleo katika sekta mbalimbali za uchumi. Mashindano hayo yalivutia maelfu ya vijana kutoka sehemu mbalimbali za Tanzania, ambapo zaidi ya waombaji 7,800 waliwasilisha bunifu zao, huku washiriki 100 bora wakichaguliwa kuendelea katika hatua za juu za mashindano. Hatimaye, katika fainali za mashindano hayo, Geofrey Samuel Sanga aliibuka mshindi wa kwanza.

Kwa kushiriki katika ufadhili wa shindano hilo, APRM Tanzania imeonesha kwa vitendo umuhimu wa kushirikiana na wadau mbalimbali katika kujenga mazingira yanayowawezesha vijana kutumia maarifa, ubunifu na teknolojia kama nyenzo za maendeleo. Ushiriki huo ulihusisha mchakato mzima wa mashindano pamoja na kutoa udhamini wa kufanikisha utekelezaji wa programu hiyo.
‘Tunaamini vijana si wanufaika wa maendeleo pekee, bali ni washiriki wakuu wa kuyabuni na kuyaendesha. Ndiyo maana APRM Tanzania inaendelea kuunga mkono majukwaa yanayowawezesha vijana kuonesha uwezo wao na kutoa suluhisho kwa changamoto za maendeleo.’ Katibu Mtendaji - APRM Tanzania.
Akizungumza wakati wa kufunga rasmi Vijana Uchumi Challenge 2026, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, aliwataka vijana kuendelea kutumia ubunifu, maarifa na teknolojia kutatua changamoto za maendeleo na kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa. Alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mazingira wezeshi yatakayowasaidia vijana kuendeleza bunifu zao, kuzigeuza kuwa biashara zenye tija na kuongeza fursa za ajira nchini.
Aidha, aliwataka vijana kuthubutu kutumia fursa zilizopo na kuendelea kubuni suluhisho zitakazoongeza thamani katika uchumi wa Tanzania. Katika fainali hizo, Geofrey Samuel Sanga aliibuka mshindi wa kwanza, Jacob Fabian Lugwisha akashika nafasi ya pili, huku Robert Malonga akimaliza katika nafasi ya tatu.
Mbali na kutambuliwa kwa ubunifu wao, washindi hao walitunukiwa zawadi mbalimbali ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuhamasisha vijana kuendelea kubuni suluhisho zenye mchango katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.




_500_500shar-50brig-20_c1.jpeg)